Shairi

 UKWELI


Ukweli jama useme, tusikie wanadamu

Ukweli usitunyime, tunataka kufahamu

Ukweli nausimame, uongo hauna zamu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu


Ukweli kote uvume, Mbeya, Tanga hadi Lamu

Ukweli ukawe sime, ya kukata udhalimu

Ukweli ukawachome, wote wasojiheshimu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu


Ukweli kama umeme, kwa banati na ghulamu

Ukweli usiuzime, twauhitaji kaumu

Ukweli bwana Mtume, kasema jambo adhimu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu


Ukweli usiuhame, kwenye wakati mgumu

Ukweli kwa mfalme, utaitwa mnajimu

Ukweli siumeume, kwa kuhofia mabomu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu


Ukweli ndani ya gome, chungwa likaitwa ndimu

Ukweli kwanza upime, utaona umuhimu

Ukweli kama kipome, ule haishi hamu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu 


Ukweli wake waume, siku hizi ni chandimu

Ukweli wa paka shume, unakuja kwa msimu

Ukweli huwa kinyume, visipokwepo vitamu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu


Ukweli sote tuseme, waungwana wasalamu

Ukweli hapa nikome, naweka chini kalamu

Ukweli usituume, ndungu wawe mahasimu

Hata kama ni mchungu, ukweli utakalamu


Al-husayniy 

Mbeya

2022

Comments

Popular posts from this blog

MBINU ZA KUPUNGUZA KUKOPWA KATIKA BIASHARA